Skip to main content

HATIMAYE AMEOLEWA

HATIMAYE AMEOLEWA.

Kwa miaka zaidi ya kenda, urafiki tuliukoleza
Japo mbali nikaenda, pesa kuitafuta Muheza
Mupenzi alijilinda, nami penzi nikatunza
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa

Ahadi tulitukuza, penzi tusije livunja
Maneno yake yalinikuza, kama samaki alinikunja
Moyo huba alinuiza, Muheza buzi sikuonja
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa

Simu na jumbe mahabuba, zilinipata si haba
Hata sikuwaza suluba, kwa kazi zilizonikaba
Nami moyo ulinijaba, nikamwekeza hadi baba
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa.

Mara wiki ikakatika, mupenzi hapatikani
Moyo nikajipa rika, labda simu matatani
Hata mwezi ukavunjika, Sina taarifa abadani
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa

Nikafuata ushauri, kwa wahenga mashuhuri
Nipate vipi saburi, wa moyo sinaye habari
Baba kasema ni nzuri, kama nikipanga safari
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa

Mwaka ulofata julai, nikarudi Shambarai
Huku najipa tumai, nenda posa wangu Nai
Furaha isiyokinai, kwa moyo wangu jinai
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa.

Nikafika Kwao nyumbani, kwa furaha nikapokewa
Moyo ukajawa amani, langu tunda nitapewa
Nikatoa ya moyoni, kadiri nilivyojaliwa
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa

Babaye kameza mate, sautiye itoke yote
Mwanangu sikiza yote, cha mtu usikiokote
Nai kashenda fungate, na mumewe wa Katote
Leo nalia mwenyewe, hatimaye ameolewa

baraka ngeleja
0756775148

Popular posts from this blog

Curriculum Vitae (C. V)

Jana nilifika katika kituo kimoja cha afya na katika Harakati za hapaaaa na pale, nikiwa nimekaa kwenye benchi ili nipumzike kidogo. Nikiwa pale wakatokea wauguzi wawili nao wakakaa karibu yangu na wakaanza kuzungumza. Mmoja akamwambia mwenzake juu ya changamoto za ajira na jinsi alivyojitahidi kutafuta nafasi hata za kujitolea bila kufanikiwa, na yule mwenzake nae akamwambia jinsi alivyopambana mpaka kupata nafasi hiyo japo wanalipwa ila bado ni posho kidogo sana. Sasa, katika mazungumzo yao mwanzoni hayakunihusu japokuwa niliyasikiliza Si unajua tena sikio halina mlango lakini walifikia kipindi wakanishirikisha kwa namna moja ama nyingine hasa walipoanza kujadili vikwazo walivyokutana navyo. Ni vikwazo vingi ila hivi viwili vitakuhusu hata wewe pia. Wakisema cha kwanza ni kuandika barua ya kuomba ajira ama kujitolea na ilitakuwa iandikwe kwa lugha ya kiigereza na kingine ni kuandaa wasifu binafsi (c.v) inayoonesha mtiririko mzuri wa taarifa zako. Hapo sasa wakanishirikisha. Ngoja ...