ETI KISA UMEUMBIKA! NGELEJA©UPP Rabi sinipe mapenzi, sijapata wa kuyaenzi Bora n'zidishie tenzi, neleze hizi simanzi Liko wapi lile penzi, uloapa utalienzi Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba. Sote tulitii kiapo, maisha yangu ni yako Hata popote tuendapo, u mlinzi nami ni wako Hani ulipo mi nipo, ilikua ahadi yako Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba Miezi kenda yapita, mke hujanipa tunda Ndani warudi saa sita, hii tabia yanishinda N'kihoji wakunja ndita, eti mi si wa kukulinda Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba Unapenda vitu ghari, pesa magari swadakta Unasema we mzuri, vigogo wengi wadata Wajipuliza uturi, na waenda kula bata Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba Pombe wanywa nyakanyaka, nusu uchi wavaa Mwili watoa sadaka, wala huogopi zinaa Sio mabosi si vilaka, wote umewapa ridhaa Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba. Wamekuhonga na gali, sasa na ndani hulali Ndoa wachezea kamali, Kwa mora dua nasali Kama sik...