ETI KISA UMEUMBIKA!
NGELEJA©UPP
Rabi sinipe mapenzi, sijapata wa kuyaenzi
Bora n'zidishie tenzi, neleze hizi simanzi
Liko wapi lile penzi, uloapa utalienzi
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba.
Sote tulitii kiapo, maisha yangu ni yako
Hata popote tuendapo, u mlinzi nami ni wako
Hani ulipo mi nipo, ilikua ahadi yako
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba
Miezi kenda yapita, mke hujanipa tunda
Ndani warudi saa sita, hii tabia yanishinda
N'kihoji wakunja ndita, eti mi si wa kukulinda
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba
Unapenda vitu ghari, pesa magari swadakta
Unasema we mzuri, vigogo wengi wadata
Wajipuliza uturi, na waenda kula bata
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba
Pombe wanywa nyakanyaka, nusu uchi wavaa
Mwili watoa sadaka, wala huogopi zinaa
Sio mabosi si vilaka, wote umewapa ridhaa
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba.
Wamekuhonga na gali, sasa na ndani hulali
Ndoa wachezea kamali, Kwa mora dua nasali
Kama sikuwa rijali, ungesema wangu mwali
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba.
Kesho natoa talaka, unachie moyo wangu
Yanishinda yako hulka, haliwi na mmoja changu
Nasubilia labuka, anipe halali yangu
Namba nane yako figa, moyoni mwangu ni mwiba.
0756775148